11
Upendo Wa Mungu Kwa Israeli
1 “Wakati Israeli alipokuwa mtoto, nilimpenda,
nilimwita mwanangu kutoka Misri.
2 Lakini kadiri nilivyomwita Israeli,
ndivyo walivyokwenda mbali nami.
Walitoa dhabihu kwa Mabaali
na kufukiza uvumba kwa vinyago.
3 Mimi ndiye niliyemfundisha Efraimu kutembea,
nikiwashika mikono;
lakini hawakutambua
kuwa ni mimi niliyewaponya.
4 Niliwaongoza kwa kamba za huruma ya kibinadamu,
kwa vifungo vya upendo;
niliondoa nira shingoni mwao
nami nikainama kuwalisha.
5 “Je, hawatarudi Misri,
nayo Ashuru haitawatawala
kwa sababu wamekataa kutubu?
6 Panga zitametameta katika miji yao,
zitaharibu makomeo ya malango yao
na kukomesha mipango yao.
7 Watu wangu wamedhamiria kuniacha.
Hata kama wakimwita Yeye Aliye Juu Sana,
kwa vyovyote hatawainua.
8 “Efraimu, ninawezaje kukuacha?
Ee Israeli, ninawezaje kukutoa?
Nitawezaje kukutendea kama Adma?
Nitawezaje kukufanya kama Seboimu?
Moyo wangu umegeuka ndani yangu,
huruma zangu zote zimeamshwa.
9 Sitatimiza hasira yangu kali,
wala sitageuka na kumharibu Efraimu.
Kwa kuwa mimi ndimi Mungu,
wala si mwanadamu,
Aliye Mtakatifu miongoni mwenu.
Sitakuja kwa ghadhabu.
10 Watamfuata Bwana ;
atanguruma kama simba.
Wakati angurumapo,
watoto wake watakuja wakitetemeka
kutoka magharibi.
11 Watakuja wakitetemeka
kama ndege wakitoka Misri,
kama hua wakitoka Ashuru.
Nitawakalisha katika nyumba zao,”
asema Bwana .
Dhambi Ya Israeli
12 Efraimu amenizunguka kwa uongo,
nyumba ya Israeli kwa udanganyifu.
Naye Yuda ni mkaidi dhidi ya Mungu,